Siku ya 7

Kwa Jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu. Amina.

"Leo uniletee ROHO ZINAZOIHESHIMU NA KUITUKUZA HURUMA YANGU KWA NAMNA YA PEKEE, na uwazamishie katika huruma yangu. Roho hizi zilihuzunika zaidi juu ya Mateso yangu na ziliingia kwa kina zaidi katika roho yangu. Ni sura hai za Moyo wangu wenye Huruma. Roho hizi zitang'aa kwa mwangaza wa pekee katika maisha yajayo. Hakuna hata moja kati yao itakayoingia katika moto wa jehanamu. Nitamkinga kila mmoja wao kwa namna ya pekee saa ya kufa."

Yesu Mwenye Huruma Sana, ambaye Moyo wako ni Upendo wenyewe, zipokee katika makao ya Moyo wako wenye Huruma Sana roho za wale wanaosifu na kuheshimu kwa namna ya pekee ukuu wa huruma yako. Roho hizi zina nguvu kwa uwezo wenyewe wa Mungu. Katikati ya mateso na shida zote, husonga mbele zikiwa na tumaini katika huruma yako; na zikiwa zimeungana nawe, ee Yesu, hubeba wanadamu wote mabegani mwao. Roho hizi hazitahukumiwa kwa ukali, bali huruma yako itazikumbatia zinapoondoka katika maisha haya.

Baba wa Milele, elekeza macho yako ya huruma juu ya roho zinazotukuza na kuheshimu sifa yako kuu kabisa, yaani huruma yako isiyopimika, na ambazo zimefungiwa ndani ya Moyo wa Yesu wenye Huruma Sana. Roho hizi ni Injili hai; mikono yao imejaa matendo ya huruma, na mioyo yao, ikiwa imefurika furaha, inakuimbia wimbo wa huruma, ee Aliye Juu kabisa! Ninakuomba, ee Mungu:

Uwaonyeshe huruma yako kulingana na tumaini na imani waliyoweka kwako. Ahadi ya Yesu itimizwe ndani yao, yeye aliyewaambia kwamba katika maisha yao, lakini hasa saa ya kufa, roho zitakazoheshimu huruma yake hii isiyopimika, yeye mwenyewe atazilinda kama utukufu wake.

Amina.

Sali Chapleti ya Huruma ya Mungu.

Kwa Jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu. Amina.