Siku ya 6

Kwa Jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu. Amina.

"Leo uniletee ROHO ZA WAPOLE NA WANYENYEKEVU NA ROHO ZA WATOTO WADOGO, na uwazamishie katika huruma yangu. Roho hizi zinafanana kwa karibu sana na Moyo wangu. Zilinitia nguvu wakati wa uchungu wangu mkali. Niliwaona kama Malaika wa duniani, watakaokesha katika madhabahu zangu. Ninamimina juu yao mafuriko yote ya neema. Ni roho mnyenyekevu tu aliye na uwezo wa kuipokea neema yangu. Naziamini roho nyenyekevu kwa namna ya pekee."

Yesu Mwenye Huruma Sana, wewe mwenyewe umesema, "Jifunzeni kwangu kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo." Zipokee katika makao ya Moyo wako wenye Huruma Sana roho zote za wapole na wanyenyekevu na roho za watoto wadogo. Roho hizi hufanya mbingu yote ishikwe na furaha kuu, nazo ni vipenzi vya Baba wa mbinguni. Ni shada lenye harufu nzuri mbele ya kiti cha enzi cha Mungu; Mungu mwenyewe hupendezwa na harufu yake. Roho hizi zina makao ya kudumu katika Moyo wako wenye Huruma Sana, ee Yesu, nazo huimba bila kukoma wimbo wa upendo na huruma.

Baba wa Milele, elekeza macho yako ya huruma juu ya roho za wapole, juu ya roho za wanyenyekevu, na juu ya watoto wadogo waliofunikwa katika makao ambayo ni Moyo wa Yesu wenye Huruma Sana. Roho hizi zinafanana kwa karibu kabisa na Mwanao. Harufu yao hupanda kutoka duniani na kufika kwenye kiti chako cha enzi. Baba wa huruma na wa wema wote, ninakuomba kwa upendo ulio nao kwa roho hizi na kwa furaha unayopata ndani yao: Ubariki ulimwengu wote, ili roho zote kwa pamoja ziimbe sifa za huruma yako kwa nyakati zisizo na mwisho.

Amina.

Kwa Jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu. Amina.